Tuesday, December 30, 2008

Chadema Out Of Competition!


Fighting for political powers in My home Constituency!


http://www.mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=8905
Date::12/29/2008
Chadema yaenguliwa uchaguzi Mbeya vijijini
Na Brandy Nelson na Peter Edson
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeenguliwa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi mdogo wa ubunge katika jimbo la Mbeya Vijijini baada ya mgombea wake, Sabwee Shitambala kuondolewa katika orodha ya wagombea kutokana na Tume ya Uchaguzi kukubali pingamizi dhidi yake lililowekwa na vyama viwili.
Kwa mujibu wa barua iliyotolewa na kusainiwa na mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi jimboni hapo, Juliana Malange mgombea huyo wa Chadema hataruhusiwa kushiriki kwenye uchaguzi huo ulioandaliwa kuziba pengo lililoachwa na Mbunge Richard Nyaulawa aliyefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu.
"Kutokana na pingamizi lililowekwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF) maombi yao yamezingatiwa na hivyo mgombea wa Chadema hataweza kuendelea na kampeni zozote za uchaguzi," inaeleza sehemu ya barua hiyo.
Uongozi wa Chadema mkoani Mbeya ulithibitisha kupokea barua yenye maamuzi hayo na kusema kuwa wanatarajia kukaa kikao baadaye jana usiku ili kujua hatima ya chama chao.
Mamia ya mashabiki wa Chadema waliokuwa wamejikusanya katika ofisi za msimamizi wa uchaguzi walionekana kujikusanya katika makundi baada ya uamuzi huo kutolewa, wengi wakiilaani hatua hiyo ya tume ya uchaguzi.
Katibu mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa alisema amesikitishwa na uamuzi huo kwa kuwa umekifanya chama hicho pamoja na wadau wengine kupoteza imani na usimamizi unaoendelea katika mchakato wa kumpata mbunge atakayerithi kiti cha Marehemu Nyaulawa.
Alisema tayari wameshapata taarifa za pingamizi dhidi ya mgombea wao kwamba limetupiliwa mbali na lile la CUF na CCM kukubalika jambo ambalo alisema limezua utata ndani ya chama chake.
"Tunajiandaa kukata rufaa ndani ya masaa 48 yajayo ili tuweze kupata haki yetu ya msingi dhidi ya mgombea wetu ambaye tunaamini kuwa alikuwa na vigezo vyote vtya kushiriki kwenye uchaguzi," alisema Dk. Slaa.
"Mimi sipo Mbeya ila tumepewa taarifa kuwa ombi letu limetupiliwa mbali, wenzetu wa CCM na CUF wamekubaliwa... jambo hili limetufanya tupoteze imani," aliongeza.
Taarifa dhidi ya pingamizi ya mgombea wa chama hicho ziliwakilishwa kwa msimamizi huyo wa uchaguzi jimboni hapo zikieleza kuwa Shitambala alikwenda kuapa katika kampuni ya uwakili badala ya mahakama ya wilaya, kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni kinyume cha sheria.
Juzi Shitambala aliwekewa pingamizi na vyama vya CUF na CCM. Chadema ilimwekea pingamizi mgombea wa CCM kwa madai kuwa alisema uongo kuhusu mahali alipozaliwa.
Vuta nikuvute hiyo ilitokea katika ofisi ya msimamizi wa uchaguzi huo ambako CUF na CCM walidai kuwa mgombea wa Chadema aliapa kinyume na taratibu za uchaguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasilisha fomu ya pingamizi hilo, mjumbe wa tume ya uchaguzi ya CUF, Hussein Mmasi alisema chama chake kiliamua kumwekea pingamizi Shitambala kutokana na kuapa katika kampuni ya uwakili badala ya Mahakama ya Wilaya.
Madai hayo ndio pia yaliyoifanya CCM kumwekea pingamizi mgombea huyo.
Wakati huohuo, CUF imesema kuwa kinazitambua mbinu zinazotumiwa na CCM katika kuhakikisha kinapata ushindi kwa kuvuruga daftari la wapiga kura na kuongeza idadi watu kwa miujiza, ikidai kuwa hiyo ndiyo silaha yao kubwa.
Akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kuzindua kampeni uchaguzi wa ubunge Mbeya Vijijini, naibu katibu mkuu wa CUF, Duni Haji alisema kuwa chama chao kinahitaji mabadiliko na kimekuwa na nafasi kubwa ya kushinda katika chaguzi mbalimbali, lakini tatizo kubwa ni mbinu chafu zinazotumiwa na CCM.
Duni alisema kuwa CCM huvuruga daftari na kuongeza idadi ya wapiga kura kimiujiza na mwisho wake huwa ni matokeo ya kura kuonyeha idadi kubwa tofauti na idadi ya waliojiandikisha.
Naibu katibu huyo alifafanua kuwa mbinu nyingine ni ile ya kumwaga polisi vijijini ili kuwajengea hofu wananchi.
"Mbinu zote hizo zinazotumiwa na CCM zina lengo la kuwaibia kura wapinzani huku wakijua mshindi anapotangazwa, wapinzani huenda mahakamani, lakini hurudi mikono mitupu kwa kuwa wao ndio serikali," alisema.
Alisema kuwa pamoja na CCM kutumia mbinu hizo chafu, bado CUF haitakata tama kudai haki na kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya kuacha tabia ya kuuza shahada zao.

No comments: